Mwandishi wetu
‘SUMU’ inayomwagwa na
aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema),
Dk. Wilbroad Slaa dhidi ya mgombea urais wa chama hicho, Edward Lowassa
juu ya madai ya ufisadi, yanavuruga kwa kiasi kikubwa ‘mafuriko’ ambayo
yamekuwa yakionekana katika mikutano ya kampeni.
Kabla ya kuibuka kwa Slaa, Lowassa
alikuwa kivutio kikubwa kwa wanachama na wafuasi wa vyama vinavyounda
Umoja wa Katiba ya Wanachi (Ukawa), kiasi kwamba kila tukio lake
lilikuwa likikusanya umati mkubwa, kama vile alipokwenda kuchukua fomu
za urais na mkutano wa uzinduzi wa kampeni hivi karibuni jijini Dar.
Lakini baada ya Slaa kujitokeza na
kueleza sababu hasa zilizomfanya ajiweke pembeni na siasa, maelfu ya
wafuasi wa Ukawa Tanzania nzima wamejikuta wakisita hasa kutokana na
ukweli kuwa hadi sasa, viongozi wa Ukawa na Lowassa wameshindwa kujibu
hoja hata moja juu ya madai yake yaliyoibua upya mjadala wa mustakabali
wa upinzani nchini.
Hali hiyo inathibitishwa na kujiengua
kutoka Chadema kwa wafuasi wengi wa chama hicho, ikiwa ni pamoja na hofu
ya viongozi hao kufuatia tetesi kuwa Slaa ana mpango wa kuzunguka nchi
nzima kuwaaga Watanzania ambao aliwafanyia kazi kwa takriban miaka 20.
“Viongozi wa Ukawa wameshindwa kujibu
hoja juu ya ufisadi wa Lowassa katika sakata la Richmond, hata ukimya
wake, kunawapa watu hisia kuwa kilichosemwa na Slaa kwa miaka yote ni
sahihi,” alisema kada wa Chadema, aliyejitambulisha kwa jina la Amos
Mallya, ambaye aliweka wazi kuwa yeye atamfuata Slaa.

Note: Only a member of this blog may post a comment.