WAZIRI Mkuu aliyejiuzulu na Mbunge wa Jimbo la
Monduli, Mh. Edward Ngoyai Lowassa, ameomba serikali iunde kamati
maalum kwa ajili ya kuzuia ajali za barabarani kwa kuwaita wahusika na
kujadiliana namna ambavyo Tanzania inaweza kuepukana na vifo vitokanavyo
na ajali za barabarani.
Lowassa aliyekuwa mgeni rasmi katika matembezi ya kulaani na kupinga
mauaji ya Albino ameyasema hayo katika Viwanja vya TCC Chang’ombe leo
jijini Dar baada ya kumalizika kwa matembezi ya kulaani na kupinga
mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi (Albino) yaliyoandaliwa na kikundi
cha wakimbiaji (Jogging) kinachotambulika kama Temeke Family yaliyokuwa
na kauli mbiu ya ‘MIMI ALBINO NINA HAKI YA KUISHI’ ambao wameguswa na
mauaji hayo na kuamua kuanzisha kampeni hiyo itakayokuwa endelevu kwa
kila mkoa hasa ile mikoa iliyokithiri kwa mauaji ya albino.
“Nawapongeza Albino kwa kudai haki zao na ninawashauri msifumbie
macho suala hili lakini pia ni wajibu wa kila Mtanzania kuliona jambo
hili wanalotendewa wenzetu ni jambo baya kwa kuwa linatuharibia heshima
nyumbani na duniani pia na ni unyama, haufai kwani tunaonekana sisi ni
majambazi tunaua binadamu wenezetu.
“Ingawa Albino waliokufa ni wachache, 75 si wachache kwa sababu ni
maisha ya binadamu lakini binadamu wengine wengi wamekufa kwenye ajali
za barabarani. Imekuwa kama ni mchezo, ni kama kuua kuku, kila siku
kila mahali ni mambo hayahaya.
“Tumesikia TABOA leo wameunda kamati, mimi nawapongeza kwa uamuzi
huo lakini napenda kuiomba serikali iunde hiyo kamati kwa sababu inaweza
kuwaita wahusika wenyewe na wengine. Kwa pamoja tuhakikishe tatizo
hili lisiendelee. Nawaomba Watanzania tulione jambo hili la kufa
binadamu kuwa ni jambo baya na halifai kuendelea, tuchukue hatua na
tuiombe serikali ichukue hatua zaidi,” alisema Lowassa.
Matembezi hayo yaliongozwa na Mbunge wa Wilaya ya Temeke, Mh. Abbas
Zuberi Mtemvu, Mbunge wa Kinondoni, Mh. Idd Azzan, Mbunge wa Ilala, Mh.
Mussa Azzan Zungu, Naibu Meya wa Manispaa ya Temeke, Mh. Juma Mkenga na
vikundi mbalimbali vya jogging wilaya ya Temeke na kumalizika na
burudani kutoka kwa msanii wa muziki wa kizazi kipya, Inspekta Haroun.
(Picha/Habari na Shani Ramadhani/ Gpl.)

Note: Only a member of this blog may post a comment.