Sunday, April 19, 2015

Anonymous

AJALI ZA BARABARANI ZIMEKUWA KAMA MCHEZO - LOWASSA

Mbunge wa Wilaya ya Temeke, Abbas Zuberi Mtemvu (kushoto) na Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Ngoyai Lowassa (kulia) baada ya kumaliza matembezi ya kupinga mauaji ya Albino.
Mh Lowassa akisalimiana na wabunge wa mkoa wa Dar es Salaam. Mwakilishi wa chama cha Albino akikabidhi risala kwa mgeni rasmi, Mh. Lowassa. Mwakilishi wa Kikundi cha Temeke Family Jogging ambaye pia ni msanii wa filamu za kibongo, Salim Ahmed ‘Gabo’,  akisoma risala. Mbunge wa wilaya ya Temeke, Abbas Mtemvu, akiongoza msafara wa matembezi ya kulaani na kupinga mauaji ya Albino. …Akiwa na baadhi ya watu wenye ulemavu wa ngozi (Albino) tayari kwa kuanza matembezi. Vikundi mbalimbali vya Jogging vikiongozwa na Temeke Family Jogging katika matembezi ya kulaani na kupinga mauaji ya Albino. Kikundi cha Jogging Temeke Family. Msanii wa muziki wa kizazi kipya, Inspekta Haroun,  akiburudisha.
WAZIRI Mkuu aliyejiuzulu na Mbunge wa Jimbo la Monduli, Mh. Edward Ngoyai Lowassa,  ameomba serikali iunde kamati maalum kwa ajili ya kuzuia ajali za barabarani kwa kuwaita wahusika na kujadiliana namna ambavyo Tanzania inaweza kuepukana na vifo vitokanavyo na ajali za barabarani. 

Lowassa aliyekuwa mgeni rasmi katika matembezi ya kulaani na kupinga mauaji ya Albino ameyasema hayo katika Viwanja vya TCC Chang’ombe leo jijini Dar baada ya kumalizika kwa matembezi ya kulaani na kupinga mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi (Albino) yaliyoandaliwa na kikundi cha wakimbiaji (Jogging) kinachotambulika kama Temeke Family yaliyokuwa na kauli mbiu ya ‘MIMI ALBINO NINA HAKI YA KUISHI’ ambao wameguswa na mauaji hayo na kuamua kuanzisha kampeni hiyo itakayokuwa endelevu kwa kila mkoa hasa ile mikoa iliyokithiri kwa mauaji ya albino. 

“Nawapongeza Albino kwa kudai haki zao na ninawashauri msifumbie macho suala hili lakini pia ni wajibu wa kila Mtanzania kuliona jambo hili wanalotendewa wenzetu ni jambo baya kwa kuwa linatuharibia  heshima nyumbani na duniani pia na ni unyama,  haufai kwani tunaonekana sisi ni majambazi tunaua binadamu wenezetu. 

“Ingawa Albino waliokufa ni wachache,  75 si wachache kwa sababu ni maisha ya binadamu lakini binadamu wengine wengi wamekufa kwenye ajali za barabarani.  Imekuwa kama ni mchezo,  ni kama kuua kuku, kila siku kila mahali ni mambo hayahaya. 

“Tumesikia TABOA leo wameunda kamati,  mimi nawapongeza kwa uamuzi huo lakini napenda kuiomba serikali iunde hiyo kamati kwa sababu inaweza kuwaita wahusika wenyewe na wengine.  Kwa pamoja tuhakikishe tatizo hili lisiendelee.  Nawaomba Watanzania tulione jambo hili la kufa binadamu kuwa ni jambo baya na halifai kuendelea, tuchukue hatua na tuiombe serikali ichukue hatua zaidi,” alisema Lowassa. 

Matembezi hayo yaliongozwa na Mbunge wa Wilaya ya Temeke, Mh. Abbas Zuberi Mtemvu, Mbunge wa Kinondoni, Mh. Idd Azzan, Mbunge wa Ilala, Mh. Mussa Azzan Zungu, Naibu Meya wa Manispaa ya Temeke, Mh. Juma Mkenga na vikundi mbalimbali vya jogging wilaya ya Temeke na kumalizika na burudani kutoka kwa msanii wa muziki wa kizazi kipya,  Inspekta Haroun. 
 (Picha/Habari na Shani Ramadhani/ Gpl.)

USIPITWE! JIUNGE NASI FACEBOOK

Subscribe to this Blog via Email :

TOA MAONI YAKO HAPA (MATUSI HAYARUHUSIWI)

Note: Only a member of this blog may post a comment.