KIONGOZI Mkuu wa chama kipya cha ACT-Wazalendo, Zitto Zuberi Kabwe, ambaye ni mbunge wa zamani wa Jimbo la Kigoma Kaskazini amesema tabia ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwenda kwenye mikutano na kuanza kusema watu wengine ifikie mahali washindane kwa hoja.
Kauli hiyo imekuja siku moja tu baada ya Chadema kufanya mkutano wake mkubwa katika Uwanja wa Furahisha na kusema kuwa Zitto ni msaliti ndani ya chama hicho ndiyo maana alifukuzwa na baada ya kufukuzwa ndipo akaanzisha chama chake cha ACT-Wazalendo.
Akijibu mapigo, amesema si jambo la busara kupanda majukwaani kuanza kuwaseng’enya wengine ila jambo la msingi ni kupanda kwenye majukwaa na kupambana kwa hoja ambazo zitaleta manufaa kwa jamii na taifa kwa ujumla.
Aidha Zitto ameongeza kuwa chama chake amekipeleka Mwanza ili kilelewe hapa na kifanye mambo makubwa hapa nchini kama vilivyo vyama vingine.
Katika hatua nyingine, amesema Tanzania inakabiriwa na ukosefu wa ajira kwa vijana na hii ni kutokana na viwanda ambavyo vingetoa ajira kwa vijana kuuzwa na serikali hivyo serikali hii kukosa majibu ya moja kwa moja kuhusu ukosefu wa ajira kwa vijana. Amevitaja viwanda vya Mwatex, na vingine vingi vilivyokuwepo ambavyo viliuzwa na kuwafanya vijana wengi kutaabika mtaani bila kazi.
Hata hivyo, amewaomba Watanzania kuwa pamoja naye katika kipindi hiki kigumu kwani ana imani kuwa atafanya vizuri katika siku za hivi karibuni katika maisha ya siasa na kuongeza kuwa muda ukifika vijana wote wanaoteseka mitaani watapata ajira kwani mpaka sasa hawategemei chochote katika serikali ya sasa iliyoko madarakani.

Note: Only a member of this blog may post a comment.