Sunday, March 29, 2015

Anonymous

MH. DAVID KAFULILA AANIKA MADUDU YA TRL

Waziri Kivuli wa Viwanda na Biashara, David Kafulia ameanika kasoro zilizojitokeza wakati wa manunuzi ya mabehewa 25 ya mizigo, ambazo zimo ndani ya ripoti ya awali ya uchunguzi uliofanywa na Mamlaka ya Udhibiti na Manunuzi (PPRA) ambayo pia inazungumzia ununuzi wa mabehewa 274. 

Kwa mujibu wa Kafulila, kasoro za msingi katika manunuzi zilizobainishwa kwenye ripoti hiyo ni namna zabuni ilivyotangazwa na hata upangaji wa viwango ulikuwa na mapungufu hivyo kuathiri ubora. 

Kafulila aliwaeleza waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam kuwa, amelazimika kuzungumzia kasoro hizo kwa sababu leo anasafiri kuelekea Dubai na kuwa serikali iliyopo madarakani, imebaki hatua za lala salama. 

Alisema uchunguzi wa PPRA uliangalia iwapo taratibu za manunuzi zilizoainishwa katika sheria na kanuni za manunuzi kama zilizingatiwa na kubainika kuwa mchakato wa ununuzi wa mabehewa uliofanywa na Shirika la Reli Tanzania (TRL), ulitumia fedha iliyotengwa kwenye bajeti ya mwaka wa fedha 2012/13. 

Alisema ripoti hiyo inaonyesha kuwa, kanuni na taratibu chini ya sheria ya Ununuzi wa Umma ya mwaka 2004 ilifutwa na Sheria namba 7 ya mwaka 2011 ambazo ndizo zilitumika katika manunuzi hayo. 

Pia alisema uchunguzi huo umebaini kuwa nyaraka za zabuni zote mbili zinaelekea kuwa kabla ya kutoa tuzo ya mkataba kwa mzabuni atayeonekana kukidhi masharti yaliyoainishwa kwenye nyaraka za zabuni, mzabuni huyo atatakiwa kufanyiwa uchunguzi wa kina ambao TRL haukuufanya.
TRL waliingia  mkataba na kampuni ya Hindusthan Engineering  and Industries ya India bila kujiridhisha kuhusu uwezo wake, hivyo ilikiuka kifungu cha 53 cha Sheria ya Ununuzi wa Umma na matakwa ya nyaraka za zabuni ambazo zilitaka uchunguzi ufanyike,” alisema. 

Kafulila alisema PPRA ilibaini kuwa zabuni hizo zilitangazwa kwenye magazeti ya ndani pekee bila kuyahusisha na yale ya kimataifa kama inavyoelekezwa kwenye nyongeza ya kwanza ya sheria ya manunuzi. 

Kadhalika, alisema uchunguzi ulibaini kuwa mikataba yote miwili ilisainiwa Machi 21, mwaka juzi ambapo kwa mujibu wa mikataba hiyo kifungu namba 3, kinaonyesha mabehewa yalitakiwa kuwasilishwa katika kipindi cha miezi 12 baada ya kusainiwa mikataba lakini TRL walichelewa. 

Alisema PPRA ilibaini kuwa, menejimenti ya TRL haikuwa makini kushughulikia maombi ya kuongezewa muda yaliyokuwa yanawasilishwa na kampuni hiyo.
Katika mkataba wa zabuni namba PA/113/2012-13/ME/G/OE/014 kampuni hii iliwasilisha maombi Juni 13, mwaka jana kuomba kuongezewa muda wa mkataba hadi Desemba 14, mwaka huo, TRL iliyaidhinisha Juni 16 na muda wa mkataba uliongezwa hadi Septemba 30,” alisema.
-NIPASHE

USIPITWE! JIUNGE NASI FACEBOOK

Subscribe to this Blog via Email :

TOA MAONI YAKO HAPA (MATUSI HAYARUHUSIWI)

Note: Only a member of this blog may post a comment.