UKISTAAJABU ya Musa utayaona ya
Firauni! Wakati Jeshi la Polisi Tanzania likitoa semina mbalimbali kwa
wananchi kuhusiana na ulinzi shirikishi, hali si shwari kabisa katika
maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar kutokana na uuzwaji wa pombe haramu
aina ya gongo, Risasi Jumatano linakupasha.
Mara kwa mara serikali imekuwa ikikemea
uuzwaji wa pombe hiyo inayowainua mabega wanywaji ‘makenchi’ ambapo
askari wamekuwa wakijitahidi kuzuia kwa nguvu zao zote, lakini bila
matokeo mazuri.
Ilibidi OFM ifike katika maeneo
yaliyotajwa na kuchunguza kwa kina ili kuupata ukweli wa madai ya wakazi
hao ambao wengi ni wazazi au walezi.
Maeneo yaliyotajwa kukithiri kwa kuuzwa
gongo na ambayo baadhi ya vijana huanza kunywa pombe hiyo tangu asubuhi
ni Ubungo ya Urafiki, Manzese, Mabibo, Manzese ya Tip Top na eneo la
Ubungo Maziwa.
Katika uchunguzi wa OFM, ilibaini kuwepo
kwa biashara hiyo katika vilabu vya pombe maeneo hayo ambapo pombe hiyo
huuzwa kama vinywaji vya kawaida haswa katika maduka madogo yanayouza
vyakula pamoja na vibanda maalum vinavyouza vileo vya kisasa.
OFM ilijionea uuzwaji wa pombe hiyo
ukiendelea ambapo biashara hiyo ni ya kipekee kwani watu maalum ndiyo
wanaouziwa kwa kuogopa kugundulika.
Hata hivyo, taarifa zilizotua katika
dawati la OFM zilidai kuwa, wauzaji hao hushirikiana na baadhi ya
walinzi wa serikali bila kukamatwa kwani huwapoza kwa kitu kidogo.
Siku hiyo, OFM nao walijifanya kama
wateja kwa kuwatumia watu maalum ambao ndiyo hutumika kwenye dili hilo
na kufanikiwa kuuziwa kadiri walivyohitaji.
OFM walifika katika kila eneo husika
ambapo walitakiwa kutoa kiasi cha shilingi elfu moja, baada ya kutoa
pesa hiyo wakasubiri kwa muda wa takribani dakika tano wakaletewa
kinywaji hicho kilichohifadhiwa kwenye chupa za maji safi lakini huku
muuzaji akitokea eneo ambalo mnunuzi hawezi kulijua.
Hata hivyo, baadhi ya maeneo, OFM
walishtukiwa na wauzaji hao kutokana na kutokuwa na mwonekano wa
wanywaji wa gongo waliozoeleka ambapo karibu wote wana afya dhaifu.
“Aaa! Msela, wewe siyo bwana! Nimeghairi
sasa, hatuuzi gongo hapa,” alisema muuzaji mmoja maeneo ya Ubungo ya
Urafiki na kukimbia na chupa yake baada ya kumbaini kamanda wa OFM kuwa
hakuwa ‘taipu’ ya wateja wake.

Note: Only a member of this blog may post a comment.