Sunday, August 2, 2015

Anonymous

LOWASSA wa CHADEMA Anatisha Zaidi ya Yule wa CCM! Soma Zaidi Hapa...

Kada mpya wa Chadema, Edward Lowassa jana amerejesha fomu ya kuwania urais, huku akifanikiwa kupata wadhamini milioni 1.6, zaidi ya nusu ya kura za urais ambazo chama hicho kilipata kwenye Uchaguzi Mkuu mwaka 2010.

Naibu katibu mkuu wa Chadema Zanzibar, Salum Mwalimu alisema idadi hiyo ya wadhamini inaashiria ushindi wa kishindo, kwa maelezo kuwa inakaribia idadi ya kura alizopigiwa katibu mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa alipogombea urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010.

Katika Uchaguzi huo, Dk Slaa alishika nafasi ya pili baada ya kupata kura 2,271,941 sawa na asilimia 26.34, huku Rais Jakaya Kikwete akipata kura 5,276,827 sawa na asilimia 61.17.

Lowassa alipochukua fomu za kuomba kuteuliwa kuwania urais kwa tiketi ya CCM, kabla ya kuhamia Chadema, alidhaminiwa na wanachama 870,000 nchi nzima.

Dk Slaa, ambaye hajaonekana hadharani tangu Lowassa ajiunge Chadema, jana hakuwapo kwenye ofisi za chama hicho wakati mbunge huyo wa Monduli alipokuwa akirejesha fomu.

Hakuna kiongozi aliyekuwa tayari kuzungumzia suala lake, lakini baadhi ya maofisa wa Chadema walisema wanaendelea kuchapa kazi.

Kama ilivyokuwa juzi katika hafla fupi wakati Lowassa akichukua fomu, umati mkubwa ulifurika na kusababisha Mtaa wa Ufipa uliopo Wilaya ya Kinondoni kufungwa, watu walijazana tena na safari hii umati huo ukiwa umebeba mabango ya kumsifu Waziri Mkuu huyo wa zamani.

Katika hafla ya jana, makamu mwenyekiti wa Chadema-Bara, Profesa Abdallah Safari alieleza jinsi Chadema ilivyojipanga kuchukua nchi na siyo kushinda ubunge na udiwani pekee na kwamba Lowassa amebakiza hatua mbili tu kuingia Ikulu, jambo walilodai kuwa limeichanganya CCM.

Wakati Lowassa ambaye alitangaza rasmi kujiondoa CCM na kujiunga na Chadema Julai 28 mwaka huu akisubiri kupitishwa na Mkutano Mkuu wa chama hicho utakaofanyika Agosti 4, habari za ndani zinaeleza kuwa vigogo kadhaa wa CCM watatambulishwa katika mkutano huo.

Habari hizo zinaeleza watakaotambulishwa siku hiyo ni wenyeviti wa CCM wa mikoa, wilaya na waliokuwa wabunge wa chama hicho ambao wanamuunga mkono Lowassa.

Jana Lowassa, aliyekuwa amevaa shati jeupe na suruali nyeusi na aliyekuwa katika gari aina ya Toyota Land Cruiser VX, alifika makao makuu ya Chadema saa 9:35 alasiri akiwa pamoja na familia yake na alipokewa na umati mkubwa wa watu waliokuwa wamebeba mabango yenye ujumbe mbalimbali.

Baadhi ya ujumbe huo ni “Chini ya Lowassa umaskini haupo”, “Kwa Lowassa hata maskini atapata ajira” na “Kingunge Ngombare-Mwiru karibu Ukawa”. Kingunge ni kada mkongwe wa CCM na anamuunga mkono Lowassa.

Mbali na kubeba mabango, watu hao walikuwa wakiimba nyimbo mbalimbali za kumsifu Lowassa na kushangilia pale ilipokuwa ikitajwa mikakati ya chama hicho kushika dola.

Akieleza taratibu na kanuni za kudhamini mgombea urais, mkurugenzi wa Oganaizesheni na Mafunzo wa chama hicho, Benson Kigaira alisema mgombea urais anatakiwa kudhaminiwa na wanachama wasiopungua 200.

Naamini fomu za Lowassa zitakuwa na idadi hiyo ya wadhamini. Ila baada ya mgombea kuchukua fomu jioni yake wanachama wa Chadema, wapenzi na Watanzania walifurika katika ofisi za Kanda, mikoa na majimbo nchi nzima wakiomba kumdhamini,” Kigaira. 

Alisema wanachama hao walidhani fomu hizo zimepelekwa kila mkoa, kutokana na kuepuka kuwanyima fursa hiyo chama hicho kilipeleka fomu ili wanachama wamdhamini na kupewa masharti kuwa lazima wawe wamejiandikisha kupiga kura, wataje namba zao za simu.

USIPITWE! JIUNGE NASI FACEBOOK

Subscribe to this Blog via Email :

TOA MAONI YAKO HAPA (MATUSI HAYARUHUSIWI)

Note: Only a member of this blog may post a comment.