INATISHA! Hivi ndivyo unavyoweza
kusema mara tu unapofika katika hospitali ya serikali ya Kijitonyama,
iliyopo Sinza Mapambano jijini Dar es Salaam kwani kuna uchafu mwingi
unaoenda tofauti kabisa na mazingira yanayostahili katika kituo hicho
cha huduma za afya, Risasi Mchanganyiko linakuthibitishia.
Kitengo
Maalum cha Oparesheni Fichua Maovu (OFM) ya Global Publishers, juzikati
kilitinga katika…..zahanati hiyo kufuatia malalamiko ya muda mrefu ya
wagonjwa juu ya kutoridhishwa na usafi, hasa maeneo muhimu ya kujisaidia
haja ndogo na kubwa.
OFM ilishuhudia vyumba vya vyoo vikiwa
gizani, matundu matatu ya vyoo hivyo yakiwa yameharibika vibaya kwa
uchakavu na mbaya zaidi, kutokuwepo na maji ya kutosha.
Baadhi ya wagonjwa waliwaambia OFM kuwa
wanawake ndiyo wako kwenye hatari zaidi ya kupata maambukizi, kwa sababu
ya uchafu uliokithiri huko, kwani upo uwezekano mkubwa wa mtu kuondoka
na ugonjwa mwingine licha ya uliompeleka katika zahanati hiyo.
Makamanda
wetu waliingia kazini mara moja na kubaini ukweli kuwa mazingira ya
zahanati hiyo hayazingatii usafi, kwani katika eneo la mapokezi,
walishuhudia uchafu wa damu sakafuni na vipande vipande vya pamba vikiwa
vimezagaa chini huku wauguzi wakiendelea kutoa huduma kwa wagonjwa kama
kawaida.
Katika vyumba vya vyoo, licha ya kuwa na
giza, kulikuwa na uchafu mwingi unaomzuia mgonjwa kuingia ndani hivyo
kuwaweka katika hali ngumu wale wanaohitaji kupima haja ndogo na kubwa
kabla ya kupatiwa matibabu.
Akizungumzia hali hiyo, Mganga Mfawidhi
wa Zahanati hiyo, Lazarius Mhojah, alikiri kuwepo kwa mazingira hayo
machafu, lakini akajitetea kuwa uongozi wao una muda mfupi tangu uanze
kazi.

Note: Only a member of this blog may post a comment.