KAMA kawaida ni Ijumaa nyingine ambayo
Mapaparazi Wetu, Musa Mateja ‘Mtanashati’, Dustan Shekidele ‘Mkude
Simba’ na Mpigapicha Wetu Mkuu, Richard Bukos walijiachia viwanja
mbalimbali kusaka matukio na kuwasiliana moja kwa moja na mkuu wao
aliyekuwa makao makuu ya gazeti hili, Bamaga-Mwenge, jijini Dar es
Salaam.
Saa 3:56 usiku
SHAROBARO MVAA MLEGEZO AUNGUZWA MAKALIO
Mkuu akiwa ofisini anampigia simu Dustan Shekidele ‘Mkude Simba’ na kumtaka amjulishe kiwanja alichopo.
Makao Makuu: Shekidele nijalie hali yako kwanza.
Shekidele: Naam Mkuu wangu huku Moro hatujambo sijui huko Dar!
Makao Makuu: Dar nako ni salama, enhe haya nipe ripoti ya huko una tukio gani?
Shekidele: Mkuu niko
maeneo ya Kichangani kuna sharobaro mmoja, hawa wanyoa ‘viduku’ na
kuteremsha suruali alikuwa akiendesha bodaboda kisharobaro si imemshinda
wakati akikata kona ya Mbuyuni na kulivaa banda la chipsi la mama
Abdul.
Makao Makuu: Duh! Hali ilikuwaje hapo sasa?
Shekidele: Mkuu huyu sharobaro kaungua vibaya na mafuta ya chipsi hasa sehemu za makalio yaani ni balaa!
Makao Makuu: Huo msala, vipi mama Abdul anasemaje?
Shekidele: Kachachamaa anataka kulipwa vitu vyake ndipo jamaa mmoja kaenda kumuita diwani wa hili eneo, John Waziri aje kuwasuluhisha.
Makao Makuu: Sawa Shekidele piga kazi ngoja nimcheki Musa Mateja.
Shekidele: Sawa Mkuu.
Saa 4:56 usiku
WAREMBO WACHANJANA VIWEMBE KISA, WEMA KUKATWA UBUNGE SINGIDA
Makao Makuu: Halooo, halooo Mateja uko wapi kijana wangu?
Mateja: Mkuu nilikuwa
Maisha Basement lakini nimepigiwa simu niende Ukumbi wa Mashujaa Grill
and Lounge kuna mtu kaniambia kuna tukio la wadada kuchanjana na
viwembe.
Makao Makuu: Enhe natumai umefika eneo la tukio nini kinaendelea?
Mateja: Mkuu ni kweli
nimekutana na hilo tukio warembo wamechanjana viwembe eti kisa Wema
Sepetu jina lake kukatwa kwenye harakati za kuwania ubunge wa viti
maalum huko Singida.
Makao Makuu: Sasa ikawaje mpaka wachanjane?
Mateja: Leo si ndiyo
majibu ya wagombea viti maalum yametoka na jina la Wema limekatwa, sasa
wadada wa Timu Wema na wale wa Timu Diamond wakaanza kunangana ndipo
dada mmoja wa Timu Wema alikuwa na kiwembe kwenye pochi yake akaanza
kumchanja nacho mwilini dada wa Timu Diamond ambaye kumbe naye alikuwa
na kiwembe pia, akajibu mashambulizi ndipo mabaunsa wamewaamulia lakini
kila mmoja anatokwa damu.
Makao Makuu: Kweli hilo bonge la tukio, muhimu sana upate picha, sawa Mateja?
Mateja: Ondoa shaka Mkuu wangu.
Saa 6:12 usiku
WALIOJIFANYA KWENDA KUKESHA KWENYE FOLENI YA BVR WANASWA WAKIFANYA UFUSKA
Makao Makuu: Haya Bukos natumai uko vizuri na unanipata, uko pande zipi?
Bukos: Mkuu nimeamua
kupitia kwenye vituo vya kujiandikisha kupiga kura ‘BVR’ ambapo wapiga
kura wanajifanya kukesha kwenye foleni na sasa niko Shule ya Msingi
Makongo Juu naona wake na waume za watu wamejiachia kwa raha zao
wakijifanya kulinda foleni zao huku wengine wakiwa kwenye vichaka usiku
huu. Yaani wale walio vichakani wanafanya ufuska mtupu Mkuu.
Makao Makuu: Wapige picha tuwarushe hewani ili kuanika mambo ya aibu wanayofanya kisha wapigie simu wenzako mkapumzike.
Bukos: Sawa Mkuu nitafanya hivyo.

Note: Only a member of this blog may post a comment.