Waziri Mkuu, Mizengo Pinda,
amelezea hofu yake juu ya kuwapo kwa fitina zinazofanywa na baadhi ya
watu kwa nia ya kuwaharibia wengine katika mchakato unaoendelea wa
makada 42 wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wanaowania kuteuliwa kugombea nafasi ya urais kupitia chama hicho.
Pinda ambaye pia ni mmoja wa makada
waliochukua fomu kutaka kuteuliwa kuwa wagombea wa urais wa CCM, alisema
namna pekee ya kuwaepuka watu wanaofitinisha wenzao ni kutowaunga
mkono.
Aidha, Pinda aliwataka pia watangaza nia
wenzake watakaoshindwa katika kinyang’anyiro hicho kukubali matokeo na
kumuunga mkono yeyote atayeibuka mshindi na pia kutambua kuwa
‘asiyekubali kushindwa si mshindani’.
Pinda aliyasema hayo wakati akihutubia
kwenye viwanja vya Mashujaa mjini hapa wakati akifunga sherehe za
maadhimisho ya wiki ya Serikali za Mitaa.
Alisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwapo
kwa amani na utulivu nchini hata baada ya uchaguzi kumalizika, huku
akiwaasa wanasiasa wote kujiepusha na vitendo vya fujo kwani hazina tija
kwa taifa na kwamba siasa ni ushindani ambao kila mtu anatakiwa
akubaliane na matokeo.
“Acheni
kuweka chuki zisizo na tija, haitowasaidia. Acheni kutaka kuwafanyia
fujo wale watakaokuwa wamekubalika katika ngazi mbalimbali kutuongoza,
maana wengine kazi yao ni fitina tu na wanataka mambo yaende ovyo.
Mzalendo wa kweli ni yule anayekubali, kama kura hazikutosha hazikutosha
tu,”.
Alitoa wito pia kwa wakurugenzi wa
halmashauri zote nchini kuhakikisha kuwa wanasimamia vizuri uchaguzi
mkuu pale mchakato utakapoanza. “Agizo
langu kwa wakurugenzi, tunakwenda katika uchaguzi mkuu. Tusifanye mzaha
na chaguzi hizi, hakikisheni mnasimamia vizuri kama sheria
zinavyoelekeza na kama kanuni zinavyoelekeza,” aliongeza.
Mwenyekiti wa Jumuia ya Umoja wa Serikali za Mitaa Tanzania (ALAT) na Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Dk. Didas Masaburi, alisema baadhi ya halmashauri nchini zimefanikiwa kupunguza tatizo la uhaba wa madawati kwa zaidi ya asilimia 80.


Note: Only a member of this blog may post a comment.