Tuesday, July 21, 2015

Anonymous

MAPYA YALIYOJIRI KESI YA ASKOFU GWAJIMA!

Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima, jana alikana kutoa lugha ya matusi dhidi ya  Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, kwamba mtoto, hana akili na mpuuzi. 

Askofu Gwajima alikanusha tuhuma hizo wakati akisomewa maelezo ya awali mbele ya Hakimu Mkazi wa Wilfred Dyansobera anayesikiliza kesi hiyo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam. 

Wakili wa Serikali Mwandamizi, Joseph Maugo, alidai kuwa kati ya Machi 16 na 25, mwaka huu katika viwanja vya Tanganyika Packers, vilivyopo Kawe jijini Dar es Salaam, mshtakiwa alitoa lugha ya matusi kwamba ‘mimi Askofu Gwajima nasema askofu Pengo ni mpuuzi mmoja yule, mjinga mmoja, amekula nini yule, sijui amekula nini yule mtoto hana akili yule’ alinukuu maneno hayo. 

Alidai kuwa Askofu Gwajima alitoa maneno hayo yakufadhaisha dhidi ya Askofu Pengo na kwamba yanaweza kusababisha uvunjifu wa amani. 

Upande huo wa Jamhuri ulidai kuwa Machi 27, mwaka huu mshtakiwa alifikishwa Kituo cha Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam kwa ajili ya kuhojiwa.
Ilidaiwa kuwa alifunguliwa mashitaka na kufikishwa mahakamani dhidi ya tuhuma hizo. 

Hata hivyo, Askofu Gwajima alikana mashitaka hayo lakini alikiri majina yake, wadhifa wake, kuhojiwa Kituo cha Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, kweli kanisa lake liko Kawe na kushitakiwa mahakamani hapo.
Upande wa Jamhuri ulidai kuwa unatarajia kuita mashahidi saba na watawasilisha vielelezo vitano. 

Wakati huo huo, mahakama hiyo imepiga kalenda kusoma maelezo ya awali ya kesi inayomkabili askofu huyo na wenzake watatu, baada ya mshtakiwa wa nne kuwa mgonjwa.
Kesi hiyo itasikilizwa mbele ya Hakimu Dyansobela Agosti 10, mwaka huu.

USIPITWE! JIUNGE NASI FACEBOOK

Subscribe to this Blog via Email :

TOA MAONI YAKO HAPA (MATUSI HAYARUHUSIWI)

Note: Only a member of this blog may post a comment.