Musa mateja
Madai mazito! Mshiriki wa Kinyang’anyiro cha Miss Tanzania
2011/12 ambaye alianza harakati za kunyakua taji hilo akitokea Mkoa wa
Shinyanga na baadaye kutwaa Taji la Miss Kanda ya Ziwa, Glory Samwel
anadaiwa kumchokonoa Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’ kwa kile
kinachodaiwa kuwa ana ukaribu wa ‘kimalovee’ na mpenzi wa Zari, Nasibu
Abdul ‘Diamond Platnumz’.
Ijumaa Wikienda lilinyetishiwa habari hizo hivi karibuni na kuamua kuzifanyia kazi hatua kwa hatua, ambapo liliweza kujiridhisha kwa baadhi ya matukio ya picha ambazo mrembo huyo amekuwa akipiga na Diamond.
Mbali na picha pia kuna matukio ya sherehe za ‘bethidei’ ambazo Diamond alionekana akiwa karibu na mrembo huyo.
Ukiachilia mbali uchunguzi huo, mwanahabari wetu alimtafuta mrembo huyo kwa lengo la kutaka kujiridhisha juu ya madai hayo ambapo alikiri kuwa na ukaribu na Diamond huku akifafanua kwamba uhusiano wake na jamaa huyo si wa kimapenzi kama wengi wanavyomchukulia.
“Hizo picha za karibu zaidi ni zile ambazo tulipiga kwenye bethidei ya meneja wa Diamond aitwaye Salaam, ambayo ilifanyika pale nyumbani kwake (Salaam) Kijitonyama (Dar) hivi karibuni.
“Ni kweli watu wengi wananituhumu kuwa na uhusiano wa kimapenzi na Diamond lakini si kweli maana ninajuana naye kawaida tu,” alisema Glory.
Kwa upande wa Diamond aliliambia Ijumaa Wikienda kuwa ni kweli anamfahamu Glory ila si mpenzi wake na anachokijua ni shabiki wake kama ilivyo kwa wengine.
Alisema hata picha alizopiga naye hakuna picha za hovyo maana zilipigwa hadharani.
“Glory ni shabiki wangu wa kawaida tu kama ilivyo kwa mashabiki wangu wengine, suala la kupiga naye picha halimaanishi ni demu wangu,” alisema Diamond.

Note: Only a member of this blog may post a comment.