Zaidi ya tembo 10,000 katika Hifadhi ya Ruaha-Rungwa wamepotea ama hawajulikani walipo.
Akitangaza matokeo ya sensa ya tembo ya mwaka 2014 mjini hapa jana, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu,
alisema wataalam wa hifadhi wameshindwa kubaini waliko au nini
kimewatokea tembo hao na kulinganisha kupotea huko sawa na ilivyotokea
kwa ndege ya Malasia Machi mwaka huu ambayo haijaonekana hadi leo.
Sensa hiyo ilifanywa na Shirika la Taifa la Utafiti Wanyamapori (TAWIRI), Frankfurt Zoological Society na Vulcan Inc katika eneo la kilomita za mraba 268,692 ambazo ni sawa na asilimia 28.3 ya eneo lote la nchi, kuanzia Mei hadi Novemba 2014.
Maeneo ilikofanyika sensa hiyo ni
Serengeti, Tarangire-Manyara, Katavi-Rukwa, Burigi-Biharamulo,
Malagarasi-Muyovosi, Soulus-Mikumi na Ruaha-Ruangwa, Mkomazi na Saadani.
“Wizara
yangu inajipanga kikamilifu kujua sababu za kupotea kwa tembo hao…je?,
waliuawa au waliondoka katika eneo la hifadhi?. Kwa kawaida kama kuna
idadi kubwa ya vifo vya wanyama kama hiyo kunakuwa na mabaki ya mizoga
au mifupa kitu ambacho hakijaonekana tangu kupotea tembo hao,” alisema.
Idadi ya tembo katika Hifadhi ya Ruaha-Rungwa imepungua kutoka 20,000 mwaka 2013 hadi kufikia 8,272 mwaka 2014.
“Tembo
10,000 katika Hifadhi ya Ruaha-Rungwa hawajulikani walipo na wala
mizoga yao haijaonekana, wamepotea kama ile ndege ya Malasia. Hali hii
inatufanya kuendesha sensa nyingine majira ya kiangazi kuanzia Agosti
hadi Novemba, wataalam wanajiuliza kila siku tembo hao wamepotelea wapi,
hizi ni habari zinazosumbua,” alisema.
Aidha, alisema matokeo ya sensa hiyo pia yamebaini kuwapo kwa upungufu mkubwa katika mfumo wa ekolojia ya Ruaha-Rungwa.
Akitangaza matokeo ya ujumla ya sensa
hiyo, Nyalandu alisema imeonyesha kupungua kwa tembo kutoka 110,000
mwaka 2009 hadi 43,330 mwaka 2014.
Hata hivyo, waziri huyo alisema idadi
ya tembo imeongezeka kutoka 13,000 mwaka 2013 hadi 15,217 mwaka jana,
ongezeko ambalo ni zaidi ya tembo 2,000.

Note: Only a member of this blog may post a comment.