Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tabora, Suzana Kaganda.
Tukio la kujiua kwa askari Polisi wa kituo cha polisi Sikonge, Tabora, PC Charles Mkoyi limechukua
sura mpya baada ya ndugu kueleza utata wa majeraha aliyonayo ndugu yao
na malalamiko yaliyoelezwa na marehemu siku chache kabla ya kukutwa na
umauti.
Ndugu wa marehemu huyo wamedai kabla ya
kifo chake alilalamika kunyanyaswa na mmoja wa viongozi wa kituo hicho
tangu alipoingia kazini.
“Baadhi
ya malalamiko aliyotueleza ni kupangwa zamu zisizo na mpangilio, kwa
mfano, anakesha kazini badala ya kupumzika anatakiwa kurudi tena
kazini…muda mwingi alikuwa anachoka sana na hata alipolalamika hakuwahi
kusikilizwa na kiongozi huyo.”
Alisema utata unaanza Kituo cha Polisi
alichodaiwa alijipiga risasi kwa kuwa alitolewa haraka na kupelekwa
Hospitali ya Mkoa, huku picha zilizopigwa kwa ajili ya kuonyeshwa
familia na upelelezi, zikionyesha amekaa kwenye kiti akiwa amekumbatia
silaha.
“Tunavyofahamu
eneo lolote lenye tukio la mauaji kama hayo, mtu haruhusiwi kufika wala
kusafishwa hadi zipigwe picha na hata ndugu waone, lakini inaonekana
walimnyanyua na kumkalisha kwenye kiti na kumpiga picha, kwa muda mfupi
palisafishwa na mwili ukapelekwa Hospitali ya Mkoa. Tunajiuliza haraka
hiyo ya nini?” alihoji ndugu huyo.
Alisema kinachozua utata zaidi ni jinsi Charles
alivyojipiga risasi kwa kuwa inaonyesha risasi iliingilia nyuma na
kutokea mbele ambako kulikuwa na mfumuko mkubwa na nyuma tundu dogo,
jambo ambalo lina shaka kwa kuwa kwa uelewa wa kawaida anawezaje
kujipiga risasi kisogoni.
Ndugu hao walidai baada ya kufika kwenye
kituo hicho, walionyeshwa barua mbili zilizoandikwa na askari huyo,
moja ikiwa ya kikazi na nyingine ya familia na kwamba walisomewa kiasi
ya familia na ya kikazi haikusomwa na hawakupewa.
“Tunajua
mwili wa askari unaposafirishwa wanabeba na vitu vyake vyote, wanajua
alikuwa hajaoa, hana ndugu, wameacha vitu vyake vyote, kesho tunavunja
matanga ndiyo siku ya kugawana nguo za marehemu, kwa mazingira haya
tutagawana nini?” alihoji ndugu huyo.
Waliongeza kuwa hakukuwa na ukaribu wa polisi katika mazishi, alikuwa askari mwenzao lakini alizikwa kama raia wa kawaida.
Alisema walionana na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tabora, Suzana Kaganda
na kumueleza malalamiko yote na kuahidi kuyafanyia kazi, huku akisema
ndani ya Jeshi la Polisi kuna utaratibu wa kufikisha malalamiko yoyote
yanayohusu askari wao.
“Waambie hao ndugu waje kuniona badala ya kulalamika kwenye vyombo vya habari,” alisema Kamanda Kaganda.
-NIPASHE

Note: Only a member of this blog may post a comment.