Rais wa Tanzania na mwenyekiti wa CCM, Jakaya Kikwete.
Hali ya siasa ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) inazidi kuwa tete baada ya makundi mbalimbali ya jamii kwenda kumshawishi Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa achukue fomu ya kugombea urais.
Hali hiyo imedhihirika baada ya makada
wa chama hicho kuanza kuvurugana kwa kutoa kauli zinazopingana juu ya
wanaomtembelea Waziri Mkuu huyo wa zamani.
Hatua hiyo imekuja siku moja baada ya Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi ya CCM, Abdallah Bulembo,
kuwataka wajumbe wa Baraza la Wazazi la chama hicho kuomba radhi kwa
kitendo chao cha kwenda nyumbani kwa Lowassa mjini Dodoma na kumtaka
agombee urais.
Pamoja na Bulembo kutoa kauli hiyo, wajumbe hao wamesema hawako tayari kuomba radhi kwa sababu hawaoni sababu ya kufanya hivyo.
Wakizungumza na waandishi wa habari
mjini hapa jana, wajumbe hao wa Baraza la Wazazi wa CCM, walisema
hawataomba radhi kama walivyotakiwa na Bulembo kwa vile walikwenda kwa
Lowassa kwa hiyari yao na kwa mapenzi yao binafsi.
Katika mazungumzo yake, Lupenza alisema
viongozi walioratibu ziara hiyo ni pamoja na Katibu wa CCM Wilaya ya
Hanang, Vioroka Kajoro na Mjumbe wa baraza hilo Mkoa wa Morogoro,
Jackline Ngonyani pamoja na Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, Mkoa wa Dodoma,
Dk. Damas Mukassa.
Alisema yeye hakushawishiwa na mtu
yeyote kwenda kwa Lowassa ila aliwasikia viongozi hao wakizungumzia juu
ya ziara hiyo na kuwataka waweke jina lake kwenye orodha ya
watakaokwenda kwa Waziri Mkuu huyo wa zamani.
“Niliwasikia
wakisema kwa mzee ni saa tatu, nikawauliza mnataka kwenda wapi,
wakaniambia wanataka kwenda kumsalimia Lowassa, nikawaambia waniandike
na mimi jina.
“Kwa hiyo hakuna mtu aliyenishinikiza
na hata siku hiyo ya safari, hakuna aliyenikumbusha, kwanza waliniacha
nikaenda kwa pikipiki nikiwa nimechelewa,” Lupenza
“Ngonyani
ambaye amekaririwa na vyombo vya habari akisema alishinikizwa kwenda
kwa Lowassa, nilimkuta akiwa nyumbani kwa Lowassa akiwa amekaa kwenye
viti vya mbele kabisa.
“Hata
wakati wa kupiga picha ulipofika, Ngonyani huyo huyo ambaye sasa
ametugeuka, aliwataka wajumbe wengine wote wakae mbali aweze kupiga
picha yeye na Lowassa peke yao.
“Yaani
hata wakati tunajitambulisha huyo huyo Ngonyani alisema ametumwa na
watu wa Ruvuma kumletea salamu Lowassa, kwamba wanamsalimia, sasa
anageukaje tena?”
Kwa upande wake, Mbunge wa Korogwe Vijijini, Stephen Ngonyani ambaye ni maarufu kwa jina la Prof. Maji Marefu, alikana kuratibu safari hiyo kama ilivyodaiwa na kueleza kuwa alishirikishwa katika dakika za mwisho na akaamua kwenda.
“Wanaojitoa
katika ziara hiyo hivi sasa nadhani walifikiri wakienda pale watapewa
fedha ama magari. Mimi nimekaa kwenye hii jumuiya kwa miaka 15 sasa,
siko tayari kuchaguliwa kiongozi, marafiki wala maadui. Siko tayari
kuomba radhi kwa sababu sina kosa nililotenda, nasema sitaomba radhi,”Ngonyani.
Naye Dk. Mukassa alisema yeye aliratibu ziara hiyo kama mwenyeji wa Mkoa wa Dodoma ambaye anapafahamu nyumbani kwa Lowassa.
Alisema Sh 600,000 walizozitoa kwa ajili
ya Lowassa kuchukulia fomu ya kugombea urais, zimetokana na michango
yao wenyewe kama wanachama wa kikundi cha kusaidia wajumbe wa jumuiya
hiyo.
-MTANZANIA


Note: Only a member of this blog may post a comment.