Marais wastaafu watatu na makamu wa
zamani wa CCM jana walifanya kazi kubwa ya kukinusuru chama hicho
kuingia kwenye mgogoro uliokuwa unanukia baada ya Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kuenguliwa kwenye mbio za urais.
Kwa mara ya kwanza, wajumbe watatu wa
Kamati Kuu ya chama hicho juzi walijitokeza hadharani na kupinga uamuzi
wa chombo hicho wa kupitisha majina ya wagombea kwa njia ambazo walisema
zinazokiuka katiba ya CCM.
Kama hiyo haitoshi, jana wajumbe wa
Halmashauri Kuu walimuweka mwenyekiti wao, Rais Jakaya Kikwete kwenye
hali ngumu baada ya kuimba wimbo wa kuonyesha kuwa na imani na Lowassa,
likiwa ni tukio la kwanza la aina yake kwenye vikao vya juu vya chama na
ambalo liliashiria kuanza kupoteza utii kwa chama.
Habari kutoka ndani ya NEC zinasema kuwa
baada ya mapumziko ya chakula cha mchana, kikao hicho kilijadili kwa
kirefu sakata la kuchujwa kwa Lowassa na pande zinazohusika zilizungumza
kwa hisia kali, ndipo marais hao, Benjamin Mkapa, Ali Hassan Mwinyi,
Abeid Amani Karume na makamu mwenyekiti wa zamani, John Samuel Malecela
walipolazimika kuingilia kati.
“Ilibidi kwanza wote waliokuwa
wanagombea urais waondolewe kwenye mkutano ndipo tuanze kujadiliana,”
alisema mmoja wa wagombea ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe.
Mjumbe mwingine wa kikao hicho alisema
Malecela, Mkapa, Karume na Mwinyi walitumia maneno ya busara na
kuwatahadharisha wajumbe dhidi ya misimamo yao.
“Walituonya
kuhusu kujali masuala yetu binafsi kuliko amani ya nchi na kututaka
kuangalia sana misimamo yetu kwa kuwa inaweza kuhatarisha amani,” alisema mjumbe huyo.
Alisema wakati kikao kilipositishwa kwa
ajili ya chakula cha mchana, kuna baadhi ya wajumbe waliondoka eneo hilo
na wengine kubaki, akiwamo Lowassa ambaye hakujulikana alielekea eneo
gani kwenye jengo hilo.
Kikao cha mchana kilianza bila ya
Lowassa kuwamo na Karume alianza kuzungumza, na kufuatiwa na Malecela,
Mkapa, na Mwinyi, ambaye alipomaliza aliwashauri wajumbe kuwa waendelee
na upigaji kura kwa kuwa suala hilo limeshaeleweka.
Mkutano ulipoanza kupiga kura ndipo
Lowassa alipoingia na kukuta kazi ya upigaji kura inaendelea na hivyo
kuendelea na shughuli hiyo.
Awali, kwa mara ya kwanza, Kikwete jana
alikumbana na mapokezi ya aina yake wakati wajumbe walipomuonyesha
waziwazi kupinga uamuzi wa Kamati Kuu kwa kuimba wimbo wa kumuunga mkono
Edward Lowassa kabla ya kikao cha Halmashauri Kuu kuanza.
Hali hiyo imetokea wakati baadhi ya
wanachama wa CCM wakiwa bado hawajakubali kuenguliwa kwa Lowassa kwenye
kinyang’anyiro cha urais kwa tiketi ya CCM baada ya Kamati Kuu kupitisha
majina ya John Pombe Magufuli, Amina Salum Ali, Bernard Membe, January
Makamba na Dk Asha Rose Migiro kwa ajili ya kupigiwa kura Halmashauri
Kuu.


Note: Only a member of this blog may post a comment.