Monday, December 7, 2015

Anonymous

Kasi ya Rais John Pombe MAGUFULI Yaibua MAPYA

Kasi ya utendaji wa Rais John Magufuli, imeibua upya sakata la ubomoaji wa jengo la ghorofa 16 ambalo serikali iliamuru libomolewe baada ya kutokidhi viwango lakini viongozi walionekana kulega lega katika utekelezaji wa agizo hilo.

Azma ya kubomolewa kwa jengo hilo lililopo mtaa wa Indira Ghand na Kisutu, kunafuatia tukio la Machi 29 mwaka 2013 baada kuporomoka kwa jengo pacha lililosababisha vifo vya watu 36, na kujeruhi wengine 18.

Hata hivyo, kazi ya kubomoa imeonekana ikisuasua kwa miaka mitatu kutokana na wakandarasi wanaopewa kazi hiyo kujitoa katika hatua ya mwisho wakitoa sababu mbalimbali.

Manispaa ya Ilala sasa imetangaza kufanya kazi hiyo haraka na tayari kampuni tatu za kimataifa zimejitokeza kufanya kazi hiyo.
Akizungumza na Nipashe, Ofisa Habari wa Manispaa ya Ilala, David Langa alisema Halmashauri hiyo ipo katika hatua ya mwisho ya kumpata mkandarasi wa kufanya kazi hiyo.

Alisema mpaka sasa katika zabuni iliyotangazwa kuna kampuni tatu zilizojitokeza kutaka kazi hiyo na wako katika hatua za mwisho mwisho kumpata mshidi wa zabuni hiyo.
“Kuna mambo mengi ya kuangalia kabla ya kubomoa jengo, lazima tujiridhishe athari zitakazojitokeza katika usalama wa watu, mazingira na mali zingine,” alisema Langa.
“Muda si mrefu tutataja jina la kampuni itakayopewa kazi, ” aliongeza Langa.

Jengo hilo linamilikiwa kwa pamoja kati ya Shirika la la Nyumba la Taifa (NHC) na Ali Raza Investment, awali lilitakiwa kuvunjwa na kampuni ya kichina ya CRJ lakini ilishindikana.

Mtaalam mmoja kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambaye hakutaka jina lake litajwe, alisema ubomoaji wa jengo la aina hiyo ni kazi ngumu na hapa nchini kuna kampuni na taasisi chache zenye uwezo wa kufanya kazi hiyo.

Alisema kuna aina mbalimbali za ubomoaji salama wa majengo ya aina hiyo, lakini ina gharama kubwa.
Mtaalam huyo alisema kinachotakiwa kufanyika ni kuhakikisha jengo hilo linaporomoshwa kwa kushuka chini na si vinginevyo kwa ajili ya kuepuka madhara.

Alizitaja njia hizo kuwa ni kubomoa kwa kuondoa ghorofa moja moja kutoka juu, lakini alionya njia hiyo ina hatari ya kukosea kisha sehemu ya ghorofa kuangukia makazi ya watu.

Alisema njia nyingine ni kutumia vyombo maalum vya kukatia na kuondoa vifusi.
“Kwa kutumia njia hii inakuwa rahisi kidogo, lakini mara nyingi kunahitajika vyombo na utaalamu wa hali ya juu ambao kwa nchi yetu ni vigumu kupata,” alisema mtaalam huyo.

Alitaja njia inayofaa na yenye madhara kidogo ni ubomoaji wa mabomu ambayo inapolipuka inaporomosha jengo kwa kulishusha chini.

Alisema mabomu hayo yanategwa kulingana na urefu wa jengo, kisha yanalipuliwa kufuata mtitiriko maalum ambao hautasababisha jengo kukatika na kuanguka.
“Mabomu haya yanategwa katika nguzo za kila ghorofa, halafu yanalipuliwa kuanzia juu kushuka chini, hivyo jengo litashuka chini na halitatawanyika,” alisema mtaalam huyo.

Hata hivyo alieleza kwamba njia hiyo inawezekana pale kazi hiyo itafanywa na vikosi vya Jeshi la Ulinzi au kampuni iliyothibitika inaweza kutumia utaalam huo.

USIPITWE! JIUNGE NASI FACEBOOK

Subscribe to this Blog via Email :

TOA MAONI YAKO HAPA (MATUSI HAYARUHUSIWI)

Note: Only a member of this blog may post a comment.