Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Dk Emmanuel Nchimbi
ambaye pia alikuwa mwanamkakati katika kambi ya Edward Lowassa katika
mbio za urais, amesema kambi yake inamuunga mkono mgombea urais
aliyeteuliwa na chama kwa sababu anauzika.
Dk Nchimbi akizungumza na gazeti hili
jana alisema Dk John Magufuli ni mgombea anayeuzika tofauti na wengine
na kwamba kambi yao inamuunga mkono katika kukiwezesha chama kuendelea
kushika dola.
Alisema linapofika suala la maslahi ya
chama wote wanakuwa kitu kimoja na kwamba uwezo na utendaji wa Dk
Magufuli ni wa hali ya juu, kiasi kwamba ni rahisi kumnadi kwa wananchi.
Dk Nchimbi ambaye baada ya Kamati Kuu
kutangaza majina matano ya wanaowania kuteuliwa, yeye na wajumbe wenzake
wawili wa Kamati Kuu, Sophia Simba na Adam Kimbisa walitoka hadharani wakisema wanajitenga na maamuzi ya kamati hiyo kwa kuwa imekiuka katiba ya CCM.
Alisema baada ya vikao vya CCM
kumpitisha Dk Magufuli, kambi yao imeamua kumuunga mkono kwakuwa ni
mtendaji mzuri wa kazi anazopewa na mifano ipo mingi katika wizara
alizoziongoza.
Dk Nchimbi alitoa mifano ya utendaji wa
Dk Magufuli kwa kuwa ameweza kujenga barabara, kukamata meli za kigeni
zinazovua kwa njia haramu katika bahari ya Tanzania na kupambana na
ujenzi usiofuata sheria hasa kwenye maeneo ya barabara.


Note: Only a member of this blog may post a comment.