Saturday, April 18, 2015

Anonymous

MADAI MAZITO SHINYANGA: KATEKISTA ADAIWA....

KATEKISTA wa Kanisa la Romani Katoliki Parokia ya Mtakatifu Kalori Lwanga Jimbo la Kahama Mkoa wa Shinyanga, Samson Magoke amekanusha vikali madai mazito kwamba amekuwa akikusanya  michango kiholela bila uongozi  wa jimbo hilo kujua. 

Baadhi ya waumini wa kanisa hilo walisema wamekuwa na mgogoro na katekista huyo kwa fedha za michango ya wapiga picha wanazotozwa waingiapo kanisani kupiga picha  za matukio kama ya sakramenti kusema fedha hizo zinakwenda kufanya  kazi gani! 

Mwenyekiti wa  umoja wa wapigapicha  Wilaya  ya  Kahama, ‘Uwapika’, ’Charles  Richard Shinwa akizungumza na paparazi wetu jimboni hapo alisema:
“Tunabaguliwa, kwani tunapoingia kupiga picha kanisani, baadhi yetu tunatozwa sh. 5,000  kwa  kila mpigapicha za  kawaida mmoja, mchukua video ni sh. 10,000 mpaka 12,000  na  baisikeli ukiingia nayo ni sh.700, pikipiki 1,500.” 

Shinwa  alisisitiza  kitendo cha katekista  kufanya  ubaguzi  kwa  baadhi ya wapigapicha ambapo wapo wanaotozwa na wasiotozwa si vizuri.“Tumewekewa mistari miwili ya waaumini kupita ili wapigwe picha. Inatuchanganya wakati wa kupiga picha maana mhusika anakuwa  upande  mwingine  na sisi wapiga picha tupo upande mwingine huku tukiwa tumeshalipishwa fedha na kupewa vitambulisho  ambavyo havina mihuri na mwisho wa shughuli tunawarudishia,” alisema Shinwa.

Paparazi wetu alimtafuta katekista huyo kutoa ufafanuzi wa tozo za wapigapicha na waumini wanaopiga picha kanisani hapo ambapo alisema:“Fedha zinazotozwa ni za kusaidia wanaofanya usafi wa ndani na nje ya kanisa  licha ya kutotangaza ila ni utaratibu wa kwetu sisi viongozi tulioweka  kuanzia 2012-2013. Hatukuwashirikisha mapadri, baba paroko na  Askofu  Roderick  Minje.” 

Naye Baba Paroko wa Jimbo la Katoliki  Kahama,  Robert Lujura alipotafutwa alisema:
“Sina taarifa ya aina hiyo, nitafanya kikao na katibu wa jimbo na katekista huyo kwa maelezo  ya ufasaha kwa jambo hilo.

“Kanisa hili lina waumini na wapigapicha waingiao kanisani, kama kuna tozo bila kuwatangazia waumini  na wapigapicha  kama kutakuwa na utaratibu wa kuwatoza fedha za kuingia kanisani  ikiwa na  baiskeli  na   pikipiki si sawa.
“Hili ni jambo  ajabu kwa  katekista kujifanyia maamuzi yenye  muono  wa  kibinafsi  pasipo  kufuata  Neno la Mungu  na  utaratibu wa kanisa,” alisema baba paroko.

USIPITWE! JIUNGE NASI FACEBOOK

Subscribe to this Blog via Email :

TOA MAONI YAKO HAPA (MATUSI HAYARUHUSIWI)

Note: Only a member of this blog may post a comment.