Mshambuliaji wa Yanga, Donald Ngoma akisalimiana na Kocha wake.
Mwandishi Wetu, Dar es SalaamKAMA ulikuwa umesahau, Mwenyekiti wa Usajili wa Simba, Zacharia Hans Poppe anakumbuka kila kitu, ndiyo maana ameamua kukumbushia siku 147 za ngumi aliyopiga mshambuliaji wa Yanga, Donald Ngoma.
Ngoma alionekana akimtwanga kichwa beki Hassan Kessy katika mechi ya mzunguko wa kwanza iliyowakutanisha watani hao kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Tokea mechi hiyo ya mzunguko wa kwanza zilipokutana, hadi zinapokutana katika mechi ya mzunguko wa pili Februari 20 ambayo ni Jumamosi, tayari siku 147 zimetimia.
Hans Poppe amesema hadi Simba inakwenda kukutana na Yanga baada ya mechi yao ya Septemba 26, mwaka jana, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), halijakaa kuhakikisha suala hilo linapatiwa hukumu.
“Ushahidi kwamba alimpiga Kessy wala si jambo la kuficha, kila kitu kiko wazi na hata video zinaonyesha kabisa. Jiulize TFF wanapoendelea kuwa kimya wanamaamisha nini, wanataka iweje?” alihoji Hans Poppe.
Mara kadhaa, Hans Poppe na uongozi wa Simba kwa ujumla, wamekuwa wakisisitiza suala la TFF kuchukua hatua kutokana na suala hilo la Ngoma kumtwanga kichwa Kessy.
Tukio hilo lilitokea katika mechi iliyopita ya Ligi Kuu Bara mzunguko wa kwanza. Simba ililala kwa mabao 2-0 katika mechi hiyo.

Note: Only a member of this blog may post a comment.