Hans Mloli,Dar es Salaam
MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Yanga,
jana walianza ligi kwa kishindo baada ya kuifumua Coastal Union ya Tanga
kwa mabao 2-0, kwenye mchezo mkali uliopigwa katika Uwanja wa Taifa,
Dar.
Huu ulikuwa mchezo wa kwanza wa Yanga baada ya ligi hiyo kuanza juzi
Jumamosi na hawakufanya makosa baada ya kuibuka na pointi tatu muhimu
ambazo ni sahihi mtu akisema ‘Yanga Watamu Aisee’.
Ushindi huu wa kwanza unawafanya Yanga kuanza kwa kukaa kileleni mwa
ligi kwa kuwa hadi sasa wenyewe tu ndiyo wamefanikiwa kupata ushindi wa
mabao 2-0, huku kila timu ikiwa imeshacheza mchezo mmoja.
Mfungaji bora wa msimu uliopita, Simon Msuva, alianza kwa kasi ya
kutetea tuzo yake baada ya kuifungia Yanga bao la kwanza katika dakika
ya saba tu ya mchezo akimalizia pasi safi kutoka kwa Amissi Tambwe,
ambaye msimu uliopita alishika nafasi ya pili kwa kupachika mabao.
Msuva ambaye kwenye michezo zaidi ya 12 ya kujipima nguvu pamoja na
ile ya Kombe la Kagame, alifanikiwa kufunga bao moja tu, jana alionyesha
kiwango cha hali ya juu huku akipoteza nafasi kadhaa za wazi.
Katika dakika ya 42 ya mchezo huo, mshambuliaji aliyekuwa anasubiriwa
kwa hamu kubwa na mashabiki wa Yanga ili aonyeshe makeke yake, Donald
Ngoma, alifanya kazi nzuri baada ya kuifungia timu yake bao safi la pili
baada ya kuiwahi pasi safi ya kichwa iliyopigwa na Tambwe ambaye
alitoka kipindi cha pili na kuingia Malimi Busungu.
Bao hili la Ngoma ambaye alipiga jumla ya pasi 21, huku tatu tu
zikipotea, lilishangiliwa zaidi na mashabiki wa Yanga kwa kuwa walikuwa
wanasubiri kwa hamu kubwa kumuona mshambuliaji huyo akitupia mpira
kimiani.
“Mchezo ulikuwa mgumu sana, tulipata nafasi nyingi za kufunga lakini
tukashindwa kuzitumia, ingawa kupata ushindi wa mabao 2-0 siyo kitu
rahisi, naamini wachezaji wangu wamefanya kazi nzuri,” alisema kocha wa
Yanga, Hans van Der Pluijm.
Hata
hivyo, pamoja na kwamba huu ulikuwa mchezo wa kwanza, Yanga ambao kipa
wa zamani wa timu hiyo Manyika Peter alikuwa kwenye benchi kama kocha wa
makipa baada ya Juma Pondamali kwenda masomoni, walionekana kuwa kwenye
kiwango kizuri zaidi na kuonyesha kuwa ni timu ambayo imekaa pamoja kwa
muda mrefu.
Mabeki wa timu hiyo, wakiongozwa na Nadir Haroub ‘Cannavaro’,
walionekana kuonana vyema huku Thaban Kamusoko, ambaye alicheza kiungo
wa kukaba akionyesha kiwango kizuri sana kwa kupiga pasi 58 na kupoteza
nne.
Hata alipotoka Mwashiuya na kuingia Deus Kaseke, bado wachezaji wa Yanga walionekana kufanya kazi kubwa sana.
Tambwe pamoja na kwamba hakufunga bao lakini anashikilia rekodi ya
mchezaji aliyetoa pasi nyingi za mabao hadi sasa akiwa ameshatoa mbili,
huku akiwa amepiga jumla ya pasi sita tu na mbili zikizaa mabao.
Hata hivyo, kuonyesha kuwa mchezo huo ulikuwa na nidhamu ya hali ya juu, ulimalizika bila kadi yoyote.
“Tulishindwa kucheza vizuri kipindi cha kwanza, lakini tuliporejea
kipindi cha pili tulicheza vizuri ingawa tulishindwa kutengeneza nafasi
nyingi,” alisema Jackson Mayanja, Kocha wa Coastal Union.
Yanga iliwakilishwa na: Ally Mustapha Bathez, Mbuyu Twite, Haji Mwinyi,
Cannavaro, Kelvin Yondani, Kamusoko, Msuva, Haruna Niyonzima, Tambwe,
Ngoma a Mwashiuya.
Coastal Union: Sebwato Nicholaus, Hamad Juma, Yassin Mustapha, Ernest
Joseph, Tumba Sued, Said Jellan, Ali Ahmed Shiboli, Youssouf Sabo na
Nassor Kapama.
Monday, September 14, 2015
YANGA SC Watamu…Aisee!
USIPITWE! JIUNGE NASI FACEBOOK
TOA MAONI YAKO HAPA (MATUSI HAYARUHUSIWI)
Filed Under:
SPORTS AND ENTERTAINMENTS
on Monday, September 14, 2015

Note: Only a member of this blog may post a comment.