Wednesday, August 12, 2015

Anonymous

TRICH: Ugonjwa Hatari Unaoshambulia sehemu nyeti Kwa Wanawake na Wanaume...Ufahamu Kwa Undani Hapa!

Ugonjwa wa Trich ni ugonjwa unaosababishwa na vimelea vya jamii ya Protozoan na huathiri mrija wa kupitisha mkojo unaojulikana kama Urethra na tupu ya mwanamke (vagina).
Ugonjwa huu huwapata pia wanaume lakini huonekana zaidi kwa wanawake na daktari anaweza kumuambia mgonjwa anayeugua maradhi haya kuwa ana Trichomonas vaginalis.
Kwa upande wa wanaume wanaweza kuuepuka ugonjwa huu kutokana na kuwa na majimaji ya kwenye tezi dume na madini ya Zinc ambayo huathiri vimelea vinavyosababisha ugonjwa huu, vinavyoitwa Trichomonas Vaginalis.
UNAAMBUKIZWAJE?
Mwanamke au hata mwanaume anaweza kukumbwa na ugonjwa huu akifanya tendo la ndoa na mtu mwenye maambukizi bila kutumia kinga.
Kwa kawaida vimelea vya Trichomonas Vaginalis ni vidogo mno ni sawa na chembechembe moja ya damu nyeupe kwa upana (10 μm) ingawa wakati mwingine ukubwa waweza kutofautiana kulingana na mazingira. Wengine huuita ugonjwa huu Trichomoniasis.
Watu wenye Trich wana hatari ya kupata ugonjwa wa Ukimwi (HIV) au magonjwa mengine ya zinaa kwa sababu bakteria hawa huharibu seli aina ya Epithelium na kusababisha vidonda (Microulcerations)  katika tishu zilizo ndani ya utupu wa mwakamke.
DALILI  KWA WANAWAKE
Dalili za Trich huanza kuonekana kuanzia siku ya 4 mpaka ya 28 baada ya mtu kupata maambukizi ya ugonjwa huu. Kwa wanawake, Trich huathiri shingo ya kizazi (Cervix), mrija wa mkojo, tupu ya mwanamke, kibofu cha mkojo, tezi zinazojulikana kama Bartholin Glands na Skene Glands.–
Wanawake waliokumbwa na ugonjwa huu hutokwa na uchafu sehemu zao za siri na huwa na rangi ya njano, kijani au kijivu na huwa mzito. Dalili nyingine ni kuwa na maumivu wakati wa kujamiiana na kutoka harufu mbaya.
Mgonjwa pia hujisikia maumivu wakati wa kujisaidia haja ndogo na shingo ya kizazi huwa nyekundu lakini hili ataligundua daktari akifanya uchunguzi kwa mgonjwa.
Dalili nyingine ni kuwasha sehemu za siri, kupata maumivu chini ya kitovu.Wanawake wengine wanaweza kuwa na vimelea hivi na wakaishi navyo kwa mwaka mzima bila kugundua kama hawatakwenda kupimwa.
DALILI KWA WANAUME
Kwa upande wa wanaume, vimelea hivi vya ugonjwa huu hupatikana katika sehemu za siri nje ya mrija wa kupitisha mkojo  yaani anterior urethra, kwenye tezi dume  yaani prostate  na kwenye mirija ya kuhifadhi na kutoa mbegu za kiume kitaalamu huitwa epididymis.
Waliokumbwa na maradhi haya wanaweza kupata dalili hizi: Kuwasha na kutokwa na uchafu au majimaji kutoka kwenye uume wake au kuwa na kichomi baada ya kujisaidia haja ndogo au baada ya kutoa mbegu za kiume.
UGUNDUZI
Mgonjwa hugundulika baada ya kufanyiwa vipimo. Kipimo cha hadubini (microscope) hutumika ambapo daktari huingiza kifaa maalum katika tupu ya mwanamke kinachojulikana kama speculum na kuchukua kipimo kwa kutumia pamba maalum (cotton swab) na kupeleka maabara kuangalia kama kuna vimelea vya trichomonas vaginalis.
Daktari pia anaweza kuangalia kama kuta za ndani za tupu ya mwanamke au shingo ya kizazi zimeathirika kwa kuwa na vidonda ambavyo ni vyekundu.
Wanaume pia huchunguzwa kwa kuchukuliwa  uchafu unaotoka kwenye uume wake kwa kutumia pamba (Cotton swab) kisha kupeleka maabara kufanyia uchunguzi kwa kuoteshwa kwenye maabara  kitaalamu huitwa culture, kuangalia kama kutakuwa na uoto wa vimelea vya ugonjwa huu baada ya siku tatu.
Mwanamke pia anaweza kuchunguzwa kama ana kiwango cha tindikali (PH) kwenye tupu ya mwanamke kwa kutumia karatasi maalum ya kipimo hiki (PH paper). Magonjwa yanayobadilisha PH hii ni pamoja na trichomoniasis, bacteria vaginosis, atrophic vaginitis nk.
Vipimo vya ugonjwa huu ni vingi kama vile kipimo cha damu kuchunguza Prostate Specific Antigen (PSA): PSA ni aina ya protini  inayozalishwa na seli za tezi dume. Kipimo cha Pap smear  ambacho hupima chembechembe au seli za shingo ya kizazi ambazo huchukuliwa na kuchunguzwa kutumia darubini. Kipimo hiki pia hutumiwa katika uchunguzi wa wanawake ili kujua kama wamepata HYPERLINK “http://tanzmed.com/index.php?option=com_k2&view=item&id=75:saratani-ya-shingo-ya-kizazi-cervical-cancer&Itemid=160”saratani ya shingo ya kizazi au la.
Kuna kipimo kingine kinachoitwa Elisa for HIV ambacho huangalia maambukizi ya ugonjwa wa ukimwi, kipimo cha mkojo, cha damu, na kadhalika.
Tiba na ushauri
Tiba ya ugonjwa huu ni kutumia dawa aina ya metronidazole au flagyl. Kwa wanawake wenye ujauzito wa chini ya miezi mitatu wasitumie dawa hii na hata wale ambao wananyonyesha, badala yake wamuone daktari.
Wale walioathirika, wanashauriwa kupata tiba pamoja na wenza wao. Dawa hizi zina madhara  mbalimbali kama vile dawa ya metronidazole ambapo mgonjwa huweza kupata mzio  (allergic reaction), kichefuchefu, kukauka midomo, kuharisha, kushuka kiwango cha chembechembe nyeupe za damu (leukopenia) ambazo hutoa kinga dhidi ya magonjwa mbalimbali na hivyo kumuweka mtu kwenye hatari ya kupata maambukizi ya maradhi.
Wanawake wenye zaidi ya miaka 18 au wale wenye upungufu wa kinga mwilini wanashauriwa kufanya vipimo hivi kila mwaka mara moja.
Mgonjwa asipotibiwa mapema, anaweza kupata maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi akijamiiana na mtu mwenye maambukizi na kwa wanawake huwasababishia kuzaa watoto njiti au wenye uzito mdogo na wanaweza kupata saratani ya shingo ya kizazi na wanaume wanaweza kukumbwa na saratani ya tezi dume.
Itaendelea wiki ijayo

USIPITWE! JIUNGE NASI FACEBOOK

Subscribe to this Blog via Email :

TOA MAONI YAKO HAPA (MATUSI HAYARUHUSIWI)

Note: Only a member of this blog may post a comment.