Said Ally, Dar es Salaam
STRAIKA hatari wa Yanga,
Mzimbabwe, Donald Ngoma, ametamka kuwa katika michezo yao ya ligi ya
hivi karibuni, Azam ndiyo timu ambayo ilimtoa jasho kutokana na safu yao
ya ulinzi kujipanga imara kuhakikisha wanamzuia asiweze kuleta madhara.
Ngoma ambaye ametua Yanga akitokea FC Platinum ya Zimbabwe,
amekuwa kwenye kiwango cha hali ya juu kiasi cha kuwa mwiba mkali kwa
mabeki mbalimbali ambapo wikiendi iliyopita alifanikiwa kuiongoza timu
yake kuibuka na pointi moja baada ya kwenda sare ya mabao 2-2 dhidi ya
Azam katika mchezo uliopigwa Uwanja wa Taifa, Dar.
Ngoma mwenye mabao 12 mpaka sasa kwenye ligi, ameliambia Championi Jumatatu kuwa mchezo huo dhidi ya Azam haukuwa mwepesi kutokana na safu ya ulinzi ya Azam ikiongozwa na Pascal Wawa kujipanga vyema ndani ya kipindi chote cha mchezo kula nao sahani moja kuhakikisha hawaleti madhara katika lango lao na kuweza kuibuka na ushindi.
“Daah mchezo wetu dhidi ya Azam kwa hakika haukuwa rahisi hata kidogo kwani wale wachezaji wa Azam haswa safu yao ya ulinzi chini ya Wawa, walicheza kwa nidhamu kubwa kuhakikisha wanatuzima tusiweze kufunga na kuibuka na ushindi.
“Lakini siyo mbaya kuweza kupata sare katika mchezo huu japo hayakuwa malengo yetu kwani tulitaka kushinda lakini kwa sasa tunasahau matokeo haya na tunaanza kujipanga kwa ajili ya michezo ijayo,” alisema Ngoma ambaye alifunga bao moja kwenye mechi hiyo.
Note: Only a member of this blog may post a comment.