Wednesday, July 15, 2015

Anonymous

MAGUFULI: Mimi Siyo Mkali...Ni mpole Sana Lakini...

Mgombea urais wa CCM, Dk John Magufuli amesema akichaguliwa kuwa rais, hatamwogopa mtu wala hataacha mtu aonewe, hasa wanyonge. 
Dk Magufuli alikuwa akizungumza jana kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika Viwanja vya Zakhem, Mbagala.

Katika mkutano huo ulioandaliwa CCM mkoani Dar es Salaam, Dk Magufuli alikuwa akitoa angalizo kila mara kuwa hawezi kuzungumza sana kwa kuwa wakati wa kampeni haujafika, ingawa katika hotuba yake fupi alitoa ahadi mbalimbali zenye sura ya kampeni. 

Aliahidi kuwa atawashughulikia watendaji wa Serikali ambao ni wazembe na kuhimiza utekelezaji wa ilani ya CCM. Aliongeza kuwa hatamwonea haya mtu yeyote atakayekuwa kikwazo kwa maendeleo ya Taifa. 

“Mimi siyo mkali, mimi ni mtu mpole sana lakini nawachukia watendaji wa Serikali ambao ni wazembe, na hao ndiyo nitakao lala nao mbele,” alisema Dk Magufuli huku akishangiliwa na umati mkubwa wa watu waliohudhuria mkutano huo. 

Dk Magufuli alisisitiza kuwa atasimamia ilani ya chama ambayo imezingatia masuala ya kilimo na biashara. Alisema ilani inawalinda wafanyabiashara wadogo na wakubwa, pia kuongeza fursa za ajira kwa vijana. 

“Maendeleo hayana chama lakini maendeleo ya kweli yataletwa na CCM. Wakati wa uchaguzi ukifika mchague wabunge na madiwani wa CCM ili kukamilisha mafiga matatu,”Magufuli.

“Ukiwa na tochi inayotumia betri tatu, wewe ukaweka betri mbili halafu katikati ukaweka gunzi, hiyo tochi itawaka?” Dk Magufuli aliuliza makutano ambao nao walimjibu kwa pamoja “haiwaki”. 

Dk Magufuli, ambaye ni Waziri wa Ujenzi, aliwashukuru wananchi kwa mapokezi makubwa aliyoyapata kuanzia Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere (JNIA) hadi viwanja vya Zakhem, Mbagala.

Alisema yeye na mgombea mwenza watahakikisha wanalipa fadhila kwa vitendo, endapo watashinda Uchaguzi Mkuu ujao na kuongoza Serikali. 

“Ninawashukuru wakazi wa Dar es Salaam kwa kuweka pembeni kambi zenu na kujitokeza kutupokea wagombea wenu. Tulikuwa wagombea 42 wenye sifa sawa, na kila mmoja alikuwa na kambi yake. Kuwa na kambi siyo kosa. Lakini wote wamevunja kambi zao na kuniunga mkono ili kukipa ushindi Chama cha Mapinduzi,” alisema.

USIPITWE! JIUNGE NASI FACEBOOK

Subscribe to this Blog via Email :

TOA MAONI YAKO HAPA (MATUSI HAYARUHUSIWI)

Note: Only a member of this blog may post a comment.